UCHAGUZI MKUU WAZIDI KUNUKIA TANZANIA

Shirika la kimataifa la kutetea haki za binadamu Amnesty International limeikosoa serikali ya Tanzania kwa kutumia sheria kuminya uhuru na demokrasia. Ripoti hiyo iliyopewa jina la 'Ukandamizaji Kisheria kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Tanzania' inadai kuwa, kutoka mwezi Januari mpaka Septemba 2020, kumekuwa na ongezeko la vitendo vya ukandamizaji vinavyoelekezwa kwa vyama vya kisiasa vya upinzani, vyombo vya habari vinavyokosoa, mashirika yasiyo ya kiserikali pamoja na wanaharakati na watetezi wa haki za binaadamu. "Ukandamizaji umekuwa na athari kubwa kwenye mijadala. Inaweza kuzuia ushiriki wa raia na kuzuia uchunguzi dhidi ya mamlaka katika rekodi za haki za binadamu, katika muktadha wa uchaguzi," Inaeleza sehemu ya ripoti hiyo. chademan Kuhusu madai ya ukandamizwaji wa vyama vya upinzani, ripoti hiyo inaeleza kuwa hata kabla ya kampeni, wanasiasa wa upinzani walikuwa katika wakati mgumu kwa kuzuiliwa kufanya mikutano ya hadhara na kukamatwa mara kwa mara na polisi. "Wanasiasa wa upinzani wanaendelea kuripoti mashambulio dhidi yao, na hatua ya polisi kushindwa kuchunguza matukio hayo kwa haraka, undani na uwazi na kuchunguza, kunamaanisha kuwa uchaguzi wa Tanzania unafanyika wakati ambapo kuna ongezeko la uminywaji wa haki za wagombea na viongozi wa upinzani."

Comments